– Baada ya kuuza/kununua gari, bajaji au pikipiki, kazi haishii pale unapokabidhiwa funguo au kupokea pesa. Ni muhimu kubadili umiliki TRA kutoka kwa mmiliki wa zamani kuja kwa mmiliki mpya. Hii itawalinda dhidi ya matatizo ya kisheria ambayo huenda yalifanywa na mmiliki wa zamani au yatayofanywa na mmiliki mpya.
– Ni faida kubwa kwa mmiliki mpya kubadili umiliki TRA kwani atajihakikishia umiliki halali wa chombo alichonunua. Kisheria jina lililopo kwenye kadi ya gari / bajaji / pikipiki ndio utambulisho wa mmiliki halali wa chombo hicho. Hivyo kama umenunua chombo hicho na hujabadilisha jina la kadi kuwa lako, kisheria wewe umeazimwa chombo hicho na si mmiliki halali!
Mmiliki mpya anapo badili usajili wa kadi kuja majina yake, anajihakikishia chombo alichonunua kimetoka kwa mmiliki halali na si cha wizi au utapeli, kwani ni mmiliki halali pekee ndie anaweza kuruhusu mabadiliko ya umiliki wa chombo hicho TRA.
Bila kusahau baada ya kubadili usajili, mmiliki mpya atajihakikishia chombo anachomiliki hakina Deni TRA, kwani kama kuna deni mabadiliko hayatafanikiwa hadi mmiliki wa awali alipe deni la Gari / Bajaji / Pikipiki husika.
Utaratibu Mpya Kubadili Umiliki Vyombo Vya Moto TRA.
– Mwanzoni mwa mwaka 2025 TRA walitambulisha mfumo mpya wa kubadili umiliki wa vyombo vya moto ambao hufanyikia katika system yao online. Katika mfumo huo TIN za muuzaji na mmiliki mpya hutumika kujaza taarifaa za mabadiliko ya umiliki.
– Ili kujaza taarifa hizo kwa usahihi, utaalamu na umakini mkubwa unahitajika ili kuepuka kupoteza muda au kupata hasara kwa kulipia control namba mara mbilimbili.
– Mchakato huu ni lazima ufanyike kwa ushirikiano kati ya mmiliki wa awali na mnunuzi mpya. Hii ni kwa sababu usajili bado upo katika TIN ya mmiliki wa awali na yeye pekee ndie mwenye uwezo wa kuruhusu mabadiliko ya umiliki kutoka kwake kuja kwa mmiliki mpya.
Mambo Muhimu Katika Kubadili Usajili wa Gari / Bajaji / Pikipiki
Zinahitajika nyaraka sahihi zifuatazo ili kuepuka usumbufu wa kisheria au ucheleweshaji wa huduma kutoka kwa mamlaka husika. Hapa chini ni maelezo ya kina ya nyaraka zinazohitajika TRA na umuhimu wake.
1. Mkataba wa Mauziano ya Gari / Bajaji / Pikipiki
Mkataba wa mauziano ni ushahidi rasmi kwamba chombo cha moto kimehamishwa kutoka kwa muuzaji kwenda kwa mnunuzi. Ni muhimu mkataba huu: usainiwe na pande zote mbili (muuzaji na mnunuzi), ugongwe muhuri wa mwanasheria, uambatane na risiti ya EFD kutoka kwa mwanasheria. Kama umepewa chombo hicho kama zawadi, urithi n.k inahitajika “Certificate of Gift” yenye muhuri na EFD receipt ya mwanasheria.
2. TIN za Muuzaji na Mnunuzi
Namba ya Utambulisho wa Mlipakodi (TIN) ni hitaji la lazima katika mchakato wa kubadili umiliki wa kadi ya gari / bajaji / pikipiki. TIN ni sharti la lazima katika mifumo ya TRA na vyombo vingine vya serikali. Hakikisha TIN za pande zote mbili zipo active na sahihi.
3. Ada za TRA Kubadili Umiliki wa Gari / Bajaji / Pikipiki Tanzania
Kuna gharama kuu tatu zinazotakiwa kulipwa TRA ambazo ni Stamp Duty, Transfer Fee na Duplicate Card. Ada hizi hutofautiana kulingana na aina na bei ya chombo cha moto. Hapa Garipesa tuna kikokotoo maalum cha kupiga hesabu ya ada utakazotakiwa kulipa TRA kulingana na aina na chombo cha moto ulicho nacho. Bofya banner ya orange kutumia calculator hiyo.
Kwa kawaida gharama hizi hulipwa na mmiliki mpya wa chombo cha moto. Malipo hayo hufanyika kupitia control namba ya serikali moja kwa moja kwenda TRA. Ni vyema mmiliki mpya ahakikishe ada hizi zimelipwa kwa wakati ili kukamilisha mchakato mapema.
4. Tax Clearence Certificate (Cheti Cha Mlipa Kodi)
Ikiwa chombo husika kilisajiliwa kwa matumizi ya biashara ni lazima mmiliki wa awali awe na Cheti cha Mlipa Kodi (Tax Clearence). Cheti hiki ni uthibitisho kwamba gari / bajaji / pikipiki aliyouza haidaiwi kodi TRA. Ikiwa chombo hicho kina deni TRA, mmiliki wa awali hataweza kupata Tax Clearence hivyo hataweza kubadilisha jina la kadi kutoka kwakwe kwenda kwa mmiliki mpya.
Hitimisho
Baada ya kubadili usajili wa chombo chako cha moto, wasiliana na kampuni ya bima na mamlaka za road license U-cancel bima iliyokuwepo ili kuhakikisha huna tena majukumu yoyote ya kisheria kwa Gari / Bajaji / Pikipiki hiyo. Pia itamsaidia mmiliki mpya kuweza kuweka bima mpya kwa jina lake na muhimu kabisa kuwa na kadi ya gari inayosoma jina lake. Kubadili umiliki ni hatua muhimu ya mwisho baada ya mauzo. Usipuuzie. Kwa kufuata hatua hizi, utalinda jina lako na kuepuka matatizo ya baadaye kama faini, ajali au makosa ya barabarani yanayoweza kufanywa na mmiliki mpya.