l1bs3zu4f351t1hv1w71vkdcamgswr

Gharama Za Kubadili Umiliki Wa Gari TRA Online

– Baada ya kununua gari, kazi haishii pale unapokabidhiwa funguo. Ni muhimu kubadili umiliki TRA kutoka kwa mmiliki wa zamani kuja kwako mmiliki mpya. 

 

 

Jinsi ya Kubadili Umiliki Wa Gari Online TRA.

– Mwanzoni mwa mwaka 2025 TRA walitambulisha mfumo mpya wa kubadili umiliki wa vyombo vya moto uitwao IDRAS. Mfumo huo hutunza taarifa za umiliki wa vyombo vya moto kupitia TIN za wamiliki.

 

– Ili kubadili umiliki, mmiliki wa zamani kupitia anatakiwa aingine katika mfumo wa IDRAS, kisha kujaza taarifa za mauzo ya gari hilo kupitia TIN yake.  

 

– Ikiwa atafanikiwa kikamilifu, mfumo wa TRA utamtolea Control namba, ambayo baada ya kulipiwa umiliki hubadilika na kuhamia kwenye TIN ya mmiliki mpya. Control namba hiyo hulipiwa kwa njia za malipo ya simu au benki.
 
– Control namba ikilipiwa mmiliki mpya ataweza ku-download kadi mpya ya gari yenye jina lake kupitia akauni yake ya IDRAS iliyounganishwa na TIN yake.

Gharama & Nyaraka Muhimu Za Kubadili Umiliki wa Gari 

ili kuepuka maombi kukataliwa, au ucheleweshwaji wa huduma kutoka TRA,  Mmiliki wa zamani atatakiwa kujaza taarifa na kuambatanisha nyaraka zifuatazo:

 

1. Mkataba wa Mauziano ya Gari

Mkataba wa mauziano ni ushahidi kwamba gari limeuzwa kutoka kwa mmiliki wa zamani kwenda kwa mmiliki mpya. Ni muhimu mkataba huu:  usainiwe na pande zote mbili (muuzaji na mnunuzi), ugongwe muhuri wa mwanasheria, uambatane na risiti ya EFD kutoka kwa mwanasheria. Kama umepewa chombo hicho kama zawadi, urithi n.k itahitajika “Certificate of Gift” yenye muhuri na EFD receipt ya mwanasheria. 

 

2. TIN ya Muuzaji na Mnunuzi 

Namba ya utambulisho wa mlipakodi (TIN) ni sharti la lazima katika mfumo wa IDRAS. Hakikisha TIN za pande zote mbili zipo active na sahihi.

 

3. Tax Clearence Certificate (Cheti Cha Mlipa Kodi)

Ikiwa gari lilisajiliwa kwa matumizi ya biashara ni lazima mmiliki wa zamani awe na hati safi ya mlipa kodi (Tax Clearence).  Cheti hiki ni uthibitisho kwamba gari alilouza halidaiwi kodi TRA. Ikiwa chombo hicho kina deni TRA,  mmiliki wa zamani hataweza kupata Tax Clearence hivyo hamtaweza kubadilisha umiliki wa gari hilo.

 

4. Gharama / Ada TRA Kubadili Umiliki wa Gari 

Gharama kuu tatu zinatakiwa kulipwa TRA ni Stamp Duty, Transfer Fee na Duplicate Card. Ada hizi hutofautiana kulingana na aina na bei ya gari. 

Kwa kawaida gharama hizi hulipwa na mmiliki mpya wa gari. Malipo hufanyika mwishoni kabisa baada ya kupata control namba.

 

 Ni vyema mmiliki mpya ahakikishe ada hizi zimelipwa kwa wakati ili kuepuka faini.

 

Hapa Garipesa tuna kikokotoo maalum cha kupiga hesabu ya  ada utakazotakiwa kulipwa TRA kulingana na aina ya gari lako. 

   

Faida Kubadili Umiliki wa Gari

Kisheria jina lililopo kwenye kadi ya gari ndio utambulisho wa mmiliki halali wa chombo hicho. Hivyo kama umenunua na hujabadilisha umiliki kuwa jina lako, kisheria wewe si mmiliki halali!

 

Mmiliki mpya utajilinda dhidi ya matatizo ya kisheria ambayo huenda yalifanywa na mmiliki wa zamani. 

 

Ukibadili umiliki unajihakikishia gari ulilonunua limetoka kwa mmiliki halali, kwani ni mmiliki halali pekee ndo ataweza kuruhusu mabadiliko ya umiliki wa gari TRA.

 

Mmiliki mpya atakua amejihakikishia kuwa gari alilonunua halina Deni TRA, kwani kama kuna deni mabadiliko hayatafanikiwa hadi mmiliki wa zamani alipe deni la Gari hilo.

Hitimisho

Kubadili umiliki ni hatua muhimu baada ya mauzo, usipuuzie! Baada ya kubadili umiliki, wasiliana na kampuni ya bima U-cancel bima iliyokuwepo na uweze kukata bima mpya kwa jina lako. 

Download GariPesa App

Nunua na uza magari kirahisi kupitia simu yako.